Thursday 7 August 2014



Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma imebarikiwa kuwa na fukwe za asili ambazo hazifanani na fukwe nyingine zozote duniani.
Ikiwa fukwe hizi  zitaendelezwa zinaweza kuwa chanzo muhimu cha mapato katika wilaya mpya ya Nyasa.
Jambo la kusitikisha ni kwamba licha ya mwambao wa ziwa Nyasa kubainika kuwa na fukwe bora duniani ambazo zinaweza kufungua utalii katika ziwa Nyasa, kwa  upande wa Tanzania hadi sasa bado hakujawa na juhudi za makusudi kuhakikisha kuwa fukwe zilizopo zinaibuliwa na kuwa chanzo cha mapato.
Fukwe ya Bayi
Hata hivyo, fukwe ya Bayi iliyopo katika eneo la Ndengere kata ya Mbambabay wilayani Nyasa, imeanza kuendelezwa na mwekezaji binafsi ambaye tayari ameanzisha vivutio mbalimbali vya utalii  kuvutia watalii wengi wa ndani na nje ya nchi .
Moja ya mambo ambayo yameipandisha chati fukwe ya Bayi ni pale mwekezaji alipoamua kuanzisha utalii wa michezo ambapo hivi sasa kuna mchezo unaoitwa ndege kidogo.
Raia mmoja wa kigeni ndiye anayefundisha wazalendo kucheza mchezo huo wa ndege ambao unapendwa na watu wengi kuangalia ndege hiyo  inaporuka juu katika fukwe hiyo.
Ndege ina uwezo wa  kubeba mtu mmoja ambayo inaruka juu kwa kusaidiwa na parachuti  umbali wa meta 60 na kusafiri umbali wa kilometa 80 kwa saa
Utalii wa ndege kidogo unavutia wakazi wengi wa mwambao mwa ziwa Nyasa ambao wanatembelea fukwe ya Bayi kila siku kwa lengo la kushiriki katika aina hiyo mpya ya utalii iliyoanzishwa katika ziwa Nyasa.
Raia wa nchini Marekani ambaye ndiye aliyetengeneza ndege ndogo anasema ndege hiyo ina  uwezo wa kubeba mtu mmoja ambaye anaruka akiwa amesimama huku mwili wake ukiwa nje.
Ndege hiyo inatumia mafuta kidogo kwenye galoni la lita tano ambayo yanabebwa mgongoni, mchezaji wa mchezo huo kichwani anakuwa amevaa kofia maalumu inayomkinga na upepo akiwa angani.
Meneja wa Fukwe ya Bayi Joseph Chengula anasema ukiachia utalii wa mchezo wa ndege kidogo, mtu anayetembelea fukwe hiyo katika eneo hilo anaweza kufanya utalii katika ziwa Nyasa kwa kuangalia fukwe ya Bayi ambayo inaongoza kwa ubora katika ziwa Nyasa na kwamba mtalii pia anaweza kufanya utalii kwa kusafiri katika boti ndani ya ziwa na kuona vivutio mbalimbali vilivyopo ndani ya ziwa hilo.

0 comments:

Post a Comment