Thursday 21 August 2014


 
Katika kile kinachoonekana kutaka mawaziri washiriki vikao vya kamati za Bunge la Katiba ili kukidhi matakwa ya akidi, Rais Jakaya Kikwete amesema hakuna ulazima wa mawaziri kuambatana naye kwenye ziara zake mikoani, badala yao wawepo makatibu wakuu wa wizara kama wanahitajika.
Rais Kikwete alinukuliwa akisema ndani ya Kamati Kuu ya CCM iliyomaliza kikao chake juzi mjini hapa kwamba yeye si kikwazo cha mahudhurio kwenye kamati za Bunge hilo na kwamba hata katika ziara yake ya Morogoro hawahitaji.
“Mwenyekiti aliweka wazi kabisa kwamba hata katika ziara yake ya Morogoro watumwe makatibu wakuu wa wizara kama kuna ulazima huo,” kilisema chanzo chetu.
Hata hivyo, katika ziara yake mkoani Morogoro iliyoanza jana, Rais Kikwete aliambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Manejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani ambaye pia ni Mbunge wa Ulanga Mashariki ziara hiyo ilikoanzia.
Pia alikuwapo Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele ambaye alihudhuria tukio la uzinduzi wa mradi wa umeme vijijini katika Kijiji cha Mwaya.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye alisema: “Kamati Kuu inawahimiza wajumbe wa Bunge la Katiba, kuhudhuria vikao vya kamati na vile vya Bunge na kushiriki katika mijadala kwa kutanguliza masilahi mapana ya Taifa na hatimaye kuipatia nchi Katiba inayotarajiwa na Watanzania wote.
Akifafanua, Nnauye alisema suala la mahudhurio kwenye vikao lilizungumzwa kwenye CC na kwamba mawaziri na wajumbe wengine wa Bunge la Katiba, wametakiwa kupunguza utoro ili akidi ya wajumbe iwe inatimia wakati wa kufanya uamuzi.
Nnauye alisema tatizo la wabunge na mawaziri watoro katika vikao vya kamati linajulikana hata ndani ya CCM... “Sasa ni wakati wa kuwaambia kuwa wapunguze kazi zao nje ya Bunge maana suala la utoro ni kweli linatufikia na wabunge nawasihi sana wasiwe watu wa kutoka-toka wakati vikao vinaendelea,” alisema.
Akidi vikaoni
Suala la akidi limekuwa likikwaza kamati za Bunge Maalumu kiasi cha kusababisha baadhi kuchelewa kuanza kwa vikao na wakati mwingine kuahirishwa.
Kadhalika, baadhi ya ibara kwenye Rasimu ya Katiba zimekuwa zikikosa akidi ya theluthi mbili ya kura kutokana na utoro wa baadhi ya wajumbe, wakiwamo mawaziri ambao mara kadhaa wamelalamikiwa na wenyeviti wa kamati kwa kutohudhuria.
Agosti 18, mwaka huu Kamati namba 11 ililazimika kuweka kando kazi zake na ikafanya kile ilichokiita semina ya uelewa kwa wajumbe, baada ya akidi kutofikiwa.

0 comments:

Post a Comment