Tuesday 5 August 2014

Bibi huyo mkazi wa Kijiji cha Lundusi Kata ya Peramiho wilayani Songea Mkoa wa Ruvuma, anasema kwa miaka mingi ameishi katika kibanda hicho alichojengewa na mzungu aliyemtaja kwa jina moja la Kilibadaambaye pia anasema alikuwa akimsaidia kulima mihogo.Share

“Kila siku naomba Mwenyezi Mungu anichukue haraka ili nikapumzike kutokana na mateso ninayoyapata, lakini hofu yangu nikifa je, nitazikwa kama binadamu wengine? Ndiyo maana nimeamua kujitayarishia jeneza langu,” anasema Scholastica Mhagama (76) mwenye ulemavu wa viungo anayeishi pekee yake katika kibanda kilichoezekwa kwa nyasi.
Bibi huyo mkazi wa Kijiji cha Lundusi Kata ya Peramiho wilayani Songea Mkoa wa Ruvuma, anasema kwa miaka mingi ameishi katika kibanda hicho alichojengewa na mzungu aliyemtaja kwa jina moja la Kilibada ambaye pia anasema alikuwa akimsaidia kulima mihogo.
Anaongeza kuwa maisha yake yanategemea kukaa nje ya kibanda chake na kuomba msaada kwa watoto wanaopita ambao huwaomba wamchotee maji.
Anabainisha kuwa mara chache anaweza kutokea mtoto ambaye humchotea maji kwenye ndoo ndogo ya lita kumi ambayo huyatumia kwa matumizi ya kuoga, kupikia, kunywa na kwamba hayatoshi kufulia wala kufanya kazi nyingine hali ambayo inamsababishia kuvaa nguo chafu wakati wote.
Anasimulia kuwa huwa anapika mara chache ndani ya kibanda anacholala na hata sehemu anayolala haina kitanda, godoro wala mkeka badala yake amekuwa analala chini katika mfuko wa mbolea na kujifunika blanketi kuu kuu.
“Ona kwanza mwanangu mahali ninapolala hakuna kitanda wala mkeka, mifuko ambayo ndiyo godoro langu huwa ninaomba tu. Nahitaji msaada, sina uwezo wa kufanya kazi yoyote tangu nilipokatwa mguu wa kulia nilipokuwa darasa la tatu hadi sasa nimekuwa naishi kwa shida ingawa sasa katika uzee hali imekuwa mbaya zaidi,’’ anasema.
Ajitengenezea jeneza
Kutokana na kushindwa kupata msaada kutoka kwa ndugu na majirani zake, Scholastica ameamua kutengeneza jeneza lake kabla ya kufa akihofia kuzikwa katika mkeka kwa kuwa ameshindwa kusaidiwa akiwa hai, hivyo anaamini akifa anaweza kutupwa kama mzoga wa mnyama asiye na faida yoyote.
“Nimetengeneza kabisa jeneza langu siku nikifa wanizike humu. Naomba Mungu anichukue haraka ili kuepukana na mateso haya. Nimetengwa na jamii na majirani wanashindwa kunisaidia wanadai eti mimi ni mchawi kwa sababu watoto wangu wote wanne walikufa wakiwa wadogo. Naumia sana kusingiziwa kitu ambacho sikijui,’’ anasema kwa masikitiko.
Bibi huyo anasema kuwa aliweza kutengeza jeneza hilo baada ya kupewa Sh40,000 na mfadhili mmoja.
“Tayari nilikuwa na mbao kwangu, hivyo kazi ilikuwa kumlipa kijana fedha na kumpa mbao ili anitengenezee jeneza,” anasema.
Hata hivyo, aliitaja misaada ya haraka ambayo anahitaji ili aweze kuishi kuwa ni pamoja na baiskeli ya miguu mitatu (wheel chair) ambayo itamwezesha kutembea kwa kuwa hivi sasa amekuwa anatambaa na kupata maumivu makali kutokana na nyama iliyobakia kwenye nyonga baada ya kukatwa mguu.

0 comments:

Post a Comment