Saturday 9 August 2014


Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza kumeguka baada ya baadhi ya wabunge wake ambao ni Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, kuunga mkono kauli ya Naibu Katibu Mkuu wake, Mwigulu Nchemba.
Nchemba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha, Jumanne iliyopita akichangia wakati wa mjadala wa mabadiliko ya kanuni, alilitaka Bunge Maalumu la Katiba lijitathmini kama lina ulazima wa kuendelea wakati hakuna uhakika wa kupatikana kwa theluthi mbili.
Alisema kitendo cha Bunge hilo kukaa kwa siku 84 bila uhakika wa kupatikana kwa theluthi mbili kwa pande zote mbili inayohitajika kupitisha Rasimu ya Katiba Mpya, hakiwezi kueleweka kwa Watanzania.
Nchemba alisema ni vyema kujua idadi ya wanaoshiriki awamu ya pili ya Bunge hilo ili kutoa uthibitisho  kimahesabu kama uamuzi wa kuendelea kwa Bunge unaweza kuwa na maana.
Jana Mwigulu Nchemba alizidi kusisitiza kauli aliyoitoa akisema ni msimamo wake binafsi kama mtoto wa maskini. Alisema anatambua jinsi walipa kodi watakavyoumia, rasimu hiyo itakapokwama kupita kutokana na kukosekana kwa theluthi mbili ya pande zote.
Hata hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye  juzi alijibu akisema kauli ya Nchemba ni mtazamo wake binafsi na hakuongea kama kiongozi wa chama hicho.
Lakini jana wabunge mbalimbali wa CCM walijitokeza hadharani wakisema wanaunga mkono kauli ya Nchemba ili hesabu ijulikane badala ya kuendelea kutafuna fedha za wananchi bila tija.
Ali Keissy
Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ali Keissy, alisema msimamo wa Nchemba ndiyo msimamo sahihi ambao unapaswa kufuatwa kuliko kuendelea na Bunge wakati wakijua kuwa theluthi mbili haitapatikana.
“Kama kuna wabunge wa CCM wanaounga mkono kauli ya Mwigulu kwa asilimia 100 basi mimi naunga mkono kwa asilimia 500 na wako wabunge wengi tu wa CCM wanaunga mkono,” alisema.   
Lembeli
Mbunge wa Kahama, James Lembeli naye alisema  kuwa alichokisema Nchemba ni ukweli ambao haupingiki.

0 comments:

Post a Comment