Sunday 10 August 2014



Mgombea wa nafasi za Mwenyekiti wa Baraza la Wazee la Chadema na mweka hazina, Jimbo la Muheza mkoani Tanga, Rashid Mhina amefariki ghafla wakati akihojiwa na wapigakura.
Mhina atazikwa leo jimboni humo, ambapo Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa anatarajiwa kuongoza mazishi hayo, yatakayofanyika saa 8 mchana.
Msimamizi wa uchaguzi huo, Grace Kiwelu aliliambia gazeti hili jana kuwa tukio hilo lilitokea saa 7.30 mchana, wakati wajumbe wa mkutano huo wakiwauliza maswali wagombea hao.
Kiwelu ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), alisema katika uchaguzi huo Mhina alipata kura nane na mshindani wake alipata kura 27 kwa nafasi ya mweka hazina, huku katika nafasi ya Mwenyekiti wa Baraza la Wazee alipata kura mbili kati ya wagombea wanne hivyo kuwa wa mwisho.
“Tulianza na nafasi ya mweka hazina ambayo ilikuwa na wagombea wawili, yeye (Mhina) na Claud Noel. Walianza kwa kuulizwa maswali na kujibu, mgombea wa kwanza alikuwa Noel na Mhina alifuatia,” alisema Kiwelu.
Aliongeza: “Alipoulizwa swali la kwanza, Mhina alijibu, alipoulizwa swali la pili akapelekewa kinasa sauti ili ajibu, ndipo alipodondoka chini na kupelekwa Hospitali Teule ya Muheza kwa matibabu.”
Kiwelu alifafanua: “Niliwaeleza wanachama kwamba tunaendelea na uchaguzi na hata kama Mhina yuko hospitali wampigie kura, lakini baadaye uchaguzi ukiwa unaendelea, tuliletewa taarifa kwamba amefariki dunia.”
Alisema kuwa baada ya taarifa hizo aliwasiliana na Dk Slaa na kumweleza kilichotokea, ambapo aliwataka kuahirisha uchaguzi wa jimbo hilo hadi utakapotangazwa tena.“Nimeshtushwa sana na tukio hili kwani ni la kwanza,” alisema Kiwelu.

0 comments:

Post a Comment