Tuesday 5 August 2014

Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) Dk Edward Hosea 
Polisi imetajwa kuwa kinara kwa rushwa katika sekta zote za huduma za serikali nchini.Kwa mujibu wa muhtasari wa utafiti uliofanywa na Shirika Lisilo la Kiserikali la Twaweza, polisi inaongoza kwa asilimia 94 ikifuatiwa na sekta za kisiasa (91), afya (82) na kodi kwa asilimia 80.
Muhtasari huo uliotolewa jana baada ya utafiti wa simu uliofanyika Juni mwaka huu pekee, ulitaja sekta nyingine kuwa ni ardhi asilimia 79, elimu (70), Serikali za Mitaa (68) na maji asilimia 56.
Matokeo ya utafiti huo uliojumuisha wananchi 1,425 wa Tanzania Bara ambao walipigiwa simu kati ya Juni 9 na 25, ulizidi kubainisha kuwa nusu ya Watanzania wanaamini kuwa mashirika yasiyo ya kiserikali nayo pia yanajihusisha na rushwa.
Muhtasari huo unaoitwa Je, juhudi za serikali zimesaidia vita dhidi ya rushwa? Mtazamo wa watu kuhusu rushwa nchini Tanzania unazidi kubainisha kuwa zaidi ya robo tatu ya wananchi wanaamini rushwa imekithiri kuliko miaka 10 ya nyuma.
“Wananchi tisa kati ya 10 wanaona rushwa inayotolewa kwa polisi ni kitu cha kawaida sana,” ilisema sehemu ya muhtasari huo.
Utafiti huo ulibainisha kuwa wananchi walitoa rushwa walipokutana na polisi na kati ya watano, watatu waliombwa rushwa.
Muhtasari huo uliongeza kuwa ni wananchi wawili tu kati ya watano walilipa rushwa hiyo na wananchi asilimia mbili walitoa rushwa wenyewe bila hata kuombwa.
Aina nyingine ya rushwa iliyoshamiri ni ile inayotolewa wakati wa kutafuta kazi na mtu mmoja kati ya watatu aliombwa malipo yasiyo rasmi alipokuwa akitafuta kazi.
“Hata hivyo, mara nyingi wananchi wana misimamo imara kwenye rushwa; huombwa mara nyingi, lakini hutoa mara chache tu,” ilisema sehemu ya muhtasari huo na kuongeza;
“Mtu mmoja kati ya 10 ameripoti kuwahi kutoa rushwa kwa ajili ya kupata kazi.”
Akielezea muhtasari huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza, Rakesh Rajan alisema ni jambo la kusikitisha kuona Watanzania wanakumbana na rushwa katika maisha yao ya kila siku licha ya jitihada mbalimbali za serikali na wadau za kuitokomeza.

0 comments:

Post a Comment