Sunday 7 September 2014

PIX 1. 
Mkurugenzi wa Habari, Elimu kwa Umma na Itifaki wa Bunge Maalum la Katiba, Bw. Jossey Mwakasyuka (kushoto) akisisitiza jambo wakati wa semina iliyoandaliwa kwa ajili ya waandishi wa habari kuhusu kuimarisha Uandishi wa Habari za shughuli za Bunge iliyofanyika tarehe 6 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa African Dreams mjini Dodoma. Kulia ni Mshauri wa mambo ya Kiufundi toka Shirika la Kimataifa la UNDP, Bi. Anna Kochannesyan.

Kanuni za Bunge Maalum hususani Kanuni ya 77 inawataka waandishi wa habari kuandika habari za Bunge Maalum kwa weledi mkubwa na kuzingatia maadili ya uandishi wa habari ili kujiepusha na uandishi wenye utashi na ushabiki wa kisiasa, msukumo binafsi, chuki ama uchochezi na wakati mwingine uongo wa makusudi.
Aidha, katika Kanuni hiyo hiyo ya 77(3) inatamka bayana ya kuwa “Katibu anaweza wakati wowote kuondoa ruhusa aliyotoa kwa mwakilishi wa Chombo chochote cha habari iwapo chombo hicho kitatoa taarifa yoyote kuhusu shughuli za Bunge Maalum ambayo kwa maoni ya Bunge Maalum inapotosha ukweli au vinginevyo inakiuka Kanuni, taratibu au haki za Bunge Maalum”.
Vyombo vya habari vina haki ya kupata habari ili viweze kuhabarisha umma juu ya mambo mbalimbali yanayoendelea nchini has katika Bunge Maalum la Katiba, lakini katika kufanya hivyo waandishi wa habari wanapaswa kutenganisha kati ya siasa na uandishi wa habari, hivyo wanapaswa kubainisha na kuainisha dhana ya uandishi wa habari za kibunge wenye tija kwa taifa ambayo ni weledi katika uandishi wa habari, uelewa kuhusu matarajio ya wananchi pamoja na uelewa juu ya dhima na dhamira ya Bunge katika taifa.
Uandishi wa habari ni vema usitumiwe kama njia ya kufikia malengo ya kisiasa ama mtu binafsi, makundi au chama na kitendo cha mwanasiasa kuvaa koti la uandishi wakati ni mwanasiasa kunajenga chuki, kunaharibu heshima ya uandishi wa habari na maisha ya waandishi.
Endapo siasa zitaingizwa katika uandishi wa habari basi kuna hatari ya kuilisha jamii yetu uongo. Mfano, kifungu cha 25 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kinavyotafsiriwa kisiasa.
Bila shaka vyombo vya habari ni kama mshipa wa damu wa siasa na demokrasia nchini. Hakuna chama cha siasa kinachoweza kufanya siasa kwa ufanisi pasipo kushirikiana na vyombo vya habari, hivyo waandishi wa habari wanakuwa vijumbe wa kubeba ujumbe wa wanasiasa, kuupeleka kwa wananchi na kubeba mrejesho wa wananchi na kuupeleka kwa wanasiasa juu ya sera na mienendo yao
Akizungumza wakati wa Semina iliyoandaliwa kwa ajili ya waandishi wa habari kuhusu namna bora ya uandishi wa habari za shughuli za Bunge, semina iliyoandaliwa na Ofisi ya Habari ya Bunge kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la UNDP ambayo ilifanyika tarehe 6 Septemba, 2014 mjini Dodoma, Mkurugenzi wa Habari, Elimu kwa Umma na Itifaki wa Bunge Maalum, Bw. Jossey Mwakasyuka alisema kuwa lengo la semina hiyo ilikuwa ni kuweza   kujadiliana na kubadilishana uzoefu juu ya uandishi wa habari kwa waandishi ili kuweza kuandika habari zilizo sahihi zinazohusu Bunge hilo kwa manufaa ya taifa.
Katika semina hiyo waandishi wengi watakuwa wameelimika vya kutosha kwani ni mambo mengi yenye umuhimu yaliwasilishwa na watoa mada waliobobea katika mambo ya uandishi na siasa hali ambayo itawafanya waandishi wengi nchini kuzingatia weledi na maadili pindi wanapokuwa wanaandika habari zinazohusiana na bunge hilo ili kuhabarisha umma.
Katika semina hiyo, watoa mada waliweza kugusia mambo mbalimbali yakiwemo uandishi wa habari za Bunge na Siasa wenye tija, athari za siasa katika uandishi wa habari za Bunge, madhara ya Vyombo vya habari kutumika, miiko na maadili ya kuzingatia katika uandishi huo.

0 comments:

Post a Comment