Friday 5 September 2014


KAMPUNI ya Kuzalisha Saruji Tanzania  (TPCC) maarufu kwa jina la biashara Twiga Cement imeanza kuzalisha kokoto nyeusi za ujenzi hiyo ikiwa ni baada ya kupata mafanikio makubwa katika katika upande wa saruji.
Hayo yamebainishwa na Meneja Usambazaji wa TPCC Joseph Tumaini wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii jana jijini Dar es Salaam ambapo walishiriki katika mkutano wa wahandisi wakiwa wadhamini wakuu.
Tumaini alisema kampuni hiyo imeamua kuzalisha kokoto nyeusi kwa lengo la kuhakikisha kuwa sekta ya ujenzi wanaitendea haki kwa kuwataka watanzania kutumia bidhaa hiyo pindi ikiingia sokoni.
Alisema uzalishaji wa kokoto nyeusi unafanyika katika eneo la Lugoba Bagamoyo ambapo inapatikana kwa wingi na wanaamini kuwa jamii inayozunguka eneo la uzalishaji wataifaidika kwa upande mmoja.
“Nadhani kila mtu ni shahidi kuwa soko la saruji hatuna mpinzani hivyo katika kuliboresha zaidi tumeona tuwaletee watanzania kokoto nyeusi jambo ambalo litawarahisishia katika ujenzi”,alisema.
Meneja huyo alisema uzinduzi wa kokoto nyeusi hizo utafanyika mwezi ujao kwa lengo la kuanza kuisambaza kwa wakala mbalimbali nchini na nje ya nchi ambao wanauza bidhaa za kampuni yao.
Alisema bidhaa hiyo ya kokoto nyeusi itakuwa ikiuzwa kwa kipimo cha malori ambapo bei yake itakuwa ya kawaida kwa kila mtanzania mjenzi kuweza kununua.
Kuhusiana na ushindani uliopo katika bidhaa yao ya saruji alisema ni wakawaida jambo ambalo wanalihitaji ili kuleta ubora wa bidhaa hiyo ambayo imekuwa na mauzo mazuri nje na ndani ya nchi.
Alisema kwa sasa wanazalisha tani milioni mbili kwa mwaka kutoka tani milioni moja na laki mbili hivyo ni wazi kuwa ushindani uliopo ni wakawaida katika biashara.
Pia TPCC inajivunia kwa saruji yake kutumika katika miradi mbalimbali ya serikali kama ujenzi wa daraja la kigamboni, uwanja wa taifa, ujenzi wa barabara ya mabasi yaendao kasi, barabara ya kilwa, PSPF na Uhuru Heights.
Tumaini alisema kuna changamoto baadhi ambazo zinawakabili ambazo ni kodi ambapo waagizaji kutoka nje wamekuwa wakitozwa kodi ndogo hivyo wakati mwingine wanapunguza soko.
Alisema ni vema serikali ikaweka mazingira sawa kwa wazalishaji wote ili kuhakikisha kuwa kila mzalishaji Napata haki sawa ambayo itamuongezea mapato ambayo yatuwa na tija kwake na kwa Taifa.

0 comments:

Post a Comment