Sunday 20 July 2014


Kazi ya uokozi Shejaiya, Gaza
Inaarifiwa kuwa Wapalestina kama 50 wameuwawa katika mtaa mmoja wa Gaza katika shambulio kubwa kabisa la mizinga tangu Israil kuanza mashambulio yake.
Makubaliano ya kusitisha mapigano baina ya Israil na Hamas huko Shejaiya ili kuruhusu magari ya wagonjwa kuingia huko, yalidumu saa moja tu, na yameanza tena.
Mwandishi wa BBC ambaye ametoka Shejaiya hivi punde, anasema kabla ya mapigano kusita kwa muda mfupi, mizinga ya Israil ikifyatuliwa mfululizo na hivo kufanya jamii yote kukimbia.
Anasema nyumba nyingi sasa zimebaki kifusi tu.
Wakuu wa Palestina wanasema watu zaidi ya 400 wameuwawa Gaza katika siku 13.
Waisraili saba wamekufa, wakiwemo raia wawili.
Ripoti kutoka Qatar zinaonesha kutafanywa mkutano huko Jumapili baina ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, na rais wa Palestina, Mahmoud Abbas, katika juhudi za kutafuta makubaliano ya kudumu ya kusitisha mapigano huko Gaza.
Qatar imekuwa kama mjumbe wa Hamas.
Kiongozi wa Hamas ambaye yuko uhamishoni, Khaled Meshaal, anaishi katika nchi hiyo ya Ghuba.
Wakuu wa huko wanasema wamepokea orodha kutoka Hamas ya shuruti zake kabla ya mapigano kusitishwa.

0 comments:

Post a Comment